Friday 25 September 2015

VIUMBE VAMIZI (Invasive Species). The forgotten Evil.



Viumbe Vamizi (adui mkubwa wa ustawi wa viumbe asiye pewa kipaumbele).
Na Simiyu David
Mobile +255764843000 email: davidmsimiyu@gmail.com
Uharibifu wa makazi asili ya viumbe ni moja ya majanga makubwa ya kimazingira kuwahi kuikabili dunia. Kwa bahati mbaya madhara ya uharibifu wa makazi ya viumbe huwa ni ya muda mrefu na mara nyingi ni ya kudumu. Makazi ya asili yanapoharibiwa au kubadilishwa, viumbe wa eneo husika huwa katika hatari ya kutoweka. Mfano mzuri unapatikana katika nchi yetu, vyura wa Kihansi (Kihansi spray toads) ni vyura wasiopatikana sehemu nyingine yoyote duniani, na ni vyura wa ajabu sana, maana badala ya kutaga kama vyura wengine wao huzaa. Vyura hawa wako katika hatari ya kutoweka kwa kuwa makazi yao ya asili yalibadilishwa kutokana na mahitaji ya binadamu. Maporomoko asili yaliyokuwepo Kihansi yanatumika sasa kufua umeme na hivyo kufanya makazi ya vyura wa Kihansi yasifae tena kwa ustawi wa viumbe hawa adimu.
Shughuri za kibinadamu inatajwa kuwa ndiyo sababu kubwa kabisa ya uharibifu/ubadilishaji wa makazi asili ya viumbe. Shughuri za kilimo, uvuvi haramu, ufugaji wa mifugo mingi katika eneo moja, uchomaji misitu, ukuaji wa miji na shughuri nyingine nyingi za kibinadamu huharibu makazi ya viumbe. Mara nyingi sababu hii (shughuri za kibinadamu) ndiyo inayotiliwa mkazo sana na wanamazingira. Jitihada nyingi za serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali zimeelekezwa katika kuelimisha jamii kuhusu madhara ya shughuri mbalimbali za binadamu kwa mazingira na jinsi ya kuweka uwiano kati ya maendeleo ya watu na ustawi wa mazingira.
Baraza la kimataifa la ustawi wa viumbe (Convention on Biological Diversity) ambalo Tanzania ni mwanachama wake, linataja sababu ya pili kubwa inayosababisha uharibifu wa makazi asili ya viumbe kuwa ni viumbe vamizi (invasive species). Janga hili la viumbe vamizi halija tiliwa sana mkazo hasa katika elimu ya jinsi ya kuzuia viumbe hivi.
Viumbe vamizi ni nini?
Viumbe hai wamegawanyika katika makundi  mbalimbali, kuna kundi la mimea, kundi la wanyama, kundi la fungi n.k. Viumbe hai wanaopatikana katika eneo fulani, wanaweza kuwa ni viumbe wa asili ya eneo hilo (native species) au wanaweza wasiwe wa asili yaani wageni katika eneo hilo (exotic/alien species). Viumbe vamizi ni viumbe wasio asili katika eneo wanaloishi na ambao huongezeka idadi na kustawi pasipo udhibiti na kubadili au kuharibu ustawi wa viumbe wengine katika eneo husika. Kwa maana hiyo, aina fulani ya kiumbe anaweza akawa sio wa asili katika eneo analoishi lakini pia asiwe kiumbe vamizi, lakini viumbe vamizi wote ni viumbe wasio asili katika maeneo wanayopatikana.
Katika Tanzania, kuna viumbe vamizi vingi. Kuwepo kwa wingi wa mimea na wanyama ambao ni vamizi katika Tanzania inashangaza kutokufahamika kwake kwa watu wengi. Kwa mujibu wa global invasive species database, Tanzania ina takribani viumbe vamizi 100. Baadhi ya viumbe ambao watu wengi tunawafahamu ni samaki aina ya sangara (Lates nilotica) katika ziwa victoria, Mimea aina ya magugu maji (Eichhornia crassipes), ndege aina ya kunguru (Indian house crow), mimea aina ya mishona nguo (Bidens pilosa) na viumbe wengine wengi (tembelea www.issg.org kupata viumbe wengine vamizi katika Tanzania).










Mashona nguo (Bidens Pilosa) ni moja kati ya mimea vamizi. Picha kwa hisani ya www.agrotico.net
 
Viumbe vamizi husambazwa zaidi na binadamu kutoka eneo moja hadi jingine. Binadamu husambaza viumbe hawa mara nyingi bila kufahamu kuwa anasafirisha viumbe. Kwa mfano mvuvi anaweza kuhamisha vifaa vyake vya uvuvi kutoka eneo moja kwenda jingine bila kujua kuwa vifaa hivyo vimebeba mayai ya samaki au mbegu za mimea. Mara nyingine binadamu hujikuta amesababisha uwepo wa viumbe vamizi baada ya kusafirisha kwa makusudi kiumbe fulani bila kujua kiumbe hicho kitakuja kuwa vamizi na kuathiri ustawi wa viumbe wengine. Kwa mfano, miaka ya 1950, enzi ya utawala wa kikoloni katika Afrika Mashariki, samaki aina ya Sangara (Lates nilotica) alipandikizwa katika ziwa Viktoria kutoka katika ziwa Albert huko Uganda kwa ajili ya kuongeza chakula kwa binadamu, matokeo yake Sangara amekua ni moja ya viumbe vamizi vilivyoleta madhara makubwa sana kwa mazingira ya ziwa hilo.
Kwanini viumbe vamizi hustawi zaidi ya viumbe wengine
Ustawi wa viumbe wasio wa-asili hadi kuwa viumbe vamizi pamoja na mambo mengine husababishwa sana na kutokuwapo na maadui wa kiumbe husika katika mazingira hayo ya ugenini. Kwa mfano kama swala walioko katika hifadhi ya Serengeti wangekuwa hawana maadui zake wa asili kama samba na chui, kuna uwezekano swala hawa wakaongezeka sana idadi hadi kuathiri mfumo asili wa kiikolojia. Hivyo ni dhahiri kuwa bila mfumo wa asili wa kudhibiti usambaaji na idadi ya viumbe wageni katika eneo fulani ni dhahiri viumbe hawa wasio wenyeji watakuwa viumbe vamizi. Kwa mimea vamizi, ustawi wake hutegemeana sana na kuwepo na uharibifu wa uoto wa asili na kuacha nafasi wazi ambayo mimea hiivamizi huweza kuziba nafasi hiyo wazi kwa haraka na hivyo kuzuia urudishiaji wa uoto wa asili.
Athari za viumbe vamizi
Ziko athari mbalimbali ambazo zinaweza kuletwa na viumbe vamizi. Athari hizo ni pamoja na, kusababisha maradhi mapya katika eneo husika. Viumbe vamizi pia, ni moja ya vyanzo vikubwa sana vya kutoweka viumbe (extinction of species). Katika ziwa Viktoria kwa mfano, samaki aina ya sangara amesababisha kutoweka kwa aina takribani mia tatu (300) katika ziwa hilo.







Samaki sangara (Lates nilotica) akiwa anachuuzwa sokoni huko Uganda. Sangara ni kiumbe vamizi katika ziwa Viktoria na amesababisha kutoweka kwa jamii nyingi za viumbe katika ziwa hilo. Picha kwa hisani ya www.news.ugo.co.ug
Madhara mengine ni uharibifu na ubadilishaji wa makazi asili ya viumbe wa eneo fulani. Mfano mzuri ni magugu maji (Eichhornia crassipes) ambayo asili yake ni katika bara la Amerika ya kusini. Magugu maji yanapotanda juu ya maji, huzuia upatikanaji mzuri wa mwanga pamoja na hewa kwa viumbe waishiyo ndani ya maji.








Magugu maji yakiwa yametanda juu ya maji. Picha na vipin chandran www.apms.org
 
Athari nyingine ya viumbe vamizi ni ile ya gharama. Kama ambavyo tulishuhudia katika suala la kupambana na magugu maji, kiasi cha fedha kilichotumika ni kikubwa sana na pia muda ambao ilichukua hadi kuyapunguza magugu maji ulikua ni mrefu sana. Kwa mfano ilibidi kuingizwa nchini viumbe (hyacinth weevils) ambao walisaidia katika kuyapunguza magugu hayo katika kile kinachojulikana kama Biological control.
Tufanyaje ili kuzuia viumbe vamizi?
Sheria ya mazingira namba 20 ya mwaka 2004 67(2) na ile ya uvuvi ya mwaka 2001, zinaelekeza kuwa si ruhusa kusafirisha na kusambaza viumbe kutoka eneo moja hadi linguine bila kuwa na ruhusa maalumu. Ni dhahiri kuwa madhara ya viumbe vamizi ni makubwa sana kwa mazingira, ingawa zipo njia mbalimbali za kupambana na viumbe vamizi kama vile kutumia viumbe hai wengine kudhibiti usambaaji wake (Biological control) na pia kutumia kemikali za sumu, lakini njia bora zaidi ni kuzuia uingiaji wake. Kama kila mmoja wetu atachukua tahadhari na hivyo kutohamisha kiumbe yoyote (mnyama au mmea) bila kuwa na uhakika kuwa kiumbe yule anapatikana pia katika maeneo unayomuhamishia basi tatizo la kusambaza viumbe vamizi litakwisha. Cha muhimu pia ni kuhakikisha vifaa kama vya uvuvi vinapohamishwa kutoka eneo moja kwenda jingine vinahakikishwa kwanza hakuna mimea au kiumbe yoyote (hasa mayai) ambayo yatahama na vifaa hivyo.
Hitimisho
Viumbe wote duniani tunaishi kwa kutegemeana. Kama makazi ya viumbe (hata kama wanaonekana kwetu kuwa hawana manufaa) yataharibika, viumbe hao watakua katika hatari ya kupotea. Kiumbe anapotoweka, hata wale viumbe wengine ambao waliishi kwa kutegemea kiumbe yule pia watadhurika. Mnyororo huu utazunguka hadi ufike kwetu sisi binadamu ambao mwenyezi Mungu ametupatia akili na maarifa ya kutawala mazingira yetu. Ni wajibu wetu kupaza sauti zetu, kuhakikisha mazingira asili yanahifadhiwa kwa gharama yoyote, tuhakikishe makazi asili ya viumbe yanalindwa na hivyo kujihakikishia ustawi wa viumbe vyote. 
By the way, ASILI NI MALI.

No comments:

Post a Comment